POLISI ARUSHA YAWAOMBA WANANCHI KUIMARISHA ULINZI JIRANI KIPINDI CHA SIKUKUU

GEDSC DIGITAL CAMERAKamanda wa Polisi mkoa wa Arusha Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Liberatus Sabas
Na Rashid Nchimbi wa Jeshi la Polisi Arusha
Jeshi la Polisi mkoani hapa limetoa wito kwa wananchi wa Mkoa huu kutumia dhana ya Ulinzi jirani katika kipindi hiki cha Sikukuu ya Krismas inayotarajiwa kuanza rasmi kesho.
Wito huo umetolewa leo asubuhi na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Liberatus Sabas wakati alipokuwa anaongea na waandishi wa habari kuelezea mikakati ya Jeshi hilo katika kipindi hiki cha sikukuu.
Alisema mara nyingi katika kusherehekea baadhi ya watu huwa wanakwenda kwenye ibada na kutembelea maeneo mbalimbali huku wakiacha nyumba zao bila waangalizi hali ambayo inaweza kusababisha uhalifu kutokea.
“Ni vema kumuacha mtu nyumbani pindi wengine wanapokuwa kwenye ibada au matembezi na pia kutaarifu majirani hali ambayo haitatoa mwanya kwa wahalifu na huu ndio Ulinzi Jirani”. Alisisitiza Kamanda Sabas.
Aidha Kamanda Sabas aliwataka watumiaji wa vyombo vya usafiri barabarani wawe makini kwa kufuata sheria zote usalama barabarani na kuwataka wasiendeshe vyombo hivyo wakiwa wamelewa, huku akiwataka watembea kwa miguu wawe waangalifu na watoto wasitembee peke yao bali waambatane na wakubwa.
Kwa upande wa maeneo ya starehe aliwakumbusha wazazi wawe makini na Mabwawa ya kuogelea (Swimming Pool) yaliyopo katika hotel mbalimbali kwani kuna mengine yanakina kirefu hali ambayo inaweza kusababisha madhara kwa watoto wao.
Kuhusu kumbi za disko amewataka wamiliki wa maeneo hayo kutoruhusu idadi zaidi ya wateja tofauti na uwezo wa kumbi zao na kuwaomba wananchi wa mkoa huu watoe taarifa haraka mara baada kuona vitendo vya ukiukwaji wa sheria vinatokea katika maeneo yao.
Hata hivyo amesema Jeshi hilo limejipanga vizuri katika kudhibiti vitendo vyovyote vya uhalifu si katika kipindi hiki cha Sikukuu ya Krismas na Mwaka Mpya bali wakati wote.

0 Response to "POLISI ARUSHA YAWAOMBA WANANCHI KUIMARISHA ULINZI JIRANI KIPINDI CHA SIKUKUU "

Post a Comment

wdcfawqafwef